Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 20:48

AU yajadili mahakama ya ICC


Mkutano wa Umoja wa Afrika, Addis Ababa, Ethiopia
Mkutano wa Umoja wa Afrika, Addis Ababa, Ethiopia
Viongozi wa Umoja wa Afrika-AU- wanakutana nchini Ethiopia kuzungumzia mahakama ya kimataifa ya uhalifu-ICC- ambayo baadhi ya nchi za kiafrika zinasema haitendei haki mataifa ya Afrika.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ethiopia, Tedros Adhanom Ghebreyesus aliwaambia wanachama 54 wa AU hapo Ijumaa kuwa ICC imekuwa chombo cha kisiasa ambapo bila aibu inawalenga wa-Afrika.

Alhamis Waziri wa Sheria wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa aliishutumu ICC kwa kuwadidimiza viongozi wa Afrika huku ikifanya hatua za pole pole kuwashitaki viongozi wa magharibi.

Ukosoaji umekuja wakati mahakama hiyo yenye makao yake The Haque ikijiandaa kwa kesi ya Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta itakayoanza mwezi Novemba.

Bwana Kenyatta na naibu wake William Ruto wanakabiliwa na mashtaka ya uhalifu dhidi ya binadamu kwa shutuma za kupanga ghasia za baada ya uchaguzi mkuu wa Kenya mwaka 2007 na mwaka 2008.

Alhamis mawakili wa Kenyatta walitaka kesi hiyo ifutwe wakielezea shutuma za ukiukaji ambazo zinajumuisha manyanyaso kwa shahidi.

Bunge la Kenya lilipiga kura mwezi uliopita kutaka nchi hiyo ijitoe uanachama wa ICC. Hata hivyo Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Amina Mohamed anasema Kenya haitajaribu kushawishi nchi za Afrika kujiondoa ICC kwa wingi.

Mwanzoni mwa wiki mahakama hiyo ya dunia ilipokea uungwaji mkono kutoka makundi 130 kote Afrika. Katika barua ya wazi walisema ICC ni mahakama muhimu kwa kesi za kimataifa.

Katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Afrika, Kofi Annan pia aliitetea ICC na aliwasihi viongozi wa Afrika kutoondoa ushirikiano wao.

Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International lilisema juhudi za wa-Afrika kujitoa kutoka ICC zitakuwa na matokeo mabaya. Katika taarifa ya Alhamis kundi hilo la haki za kimataifa lilisema mahakama inatakiwa kupanua kazi zake nje ya Afrika lakini hiyo haimaanishi kwamba mashtaka ya sasa hivi ya ICC yanayojumuisha nchi za ki-Afrika yalikuwa ya uonevu.

Rais wa zamani wa Ivory Coast, Laurent Gbagbo anasubiri kesi yake kwenye mahakama hiyo ya ICC kwa mashtaka ya uhalifu dhidi ya binadamu. Rais wa Susan Omar al-Bashir anatafutwa na mahakama ya ICC kwa shutuma za uhalifu wa vita na mauaji ya halaiki katika mkoa wa Darfur nchini Sudan.

Mkutano wa AU ulianza Ijumaa kwa mikutano ya ngazi za mawaziri. Wakuu wa nchi watajumuika na mawaziri hao katika kikao cha Jumamosi mjini Addis Ababa.
XS
SM
MD
LG