Rais wa zamani wa Nigeria Olusegun Obasanjo aliwasili Senegal Jumanne jioni kuongoza ujumbe wa tume ya pamoja ya waangalizi wa Umoja wa Afrika na shirika la kijamii na maendeleo la Afrika Magharibi ECOWAS. Alipoulizwa na wanahabari ujumbe alioleta Senegal kutoka kwa Umoja wa Afrika, bwana Obasanjo alisema kazi yake ya kwanza itakuwa kufuatilia uchaguzi wa Jumapili na ya pili kuchukua hatua kama mwakilishi wa Umoja wa Afrika na ECOWAS kuzuia kile ‘kisichotakiwa kutokea nchini humo.’ Kuwasili kwake nchini humo kulikumbana na siku nyingine ya ghasia katika mji mkuu wa Dakar ambapo polisi walitawanya waandamanaji kwa gesi ya kutoa machozi na kuwazuia kuingia katikati ya mji huo. Upinzani unamtaka rais wa sasa Abdoulaye Wade ajiondoe kama mgombea urais kwa muhula wa 3 wakisema marekebisho ya katiba ya mwaka wa 2001 yanasema bayana kuwa rais anaweza kuhudumu kwa mihula miwili pekee.
Rais Obasanjo aenda Senegal akiongoza ujumbe wa tume ya waangalizi wa Umoja wa Afrika.