Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 05:18

Ajali ya Zanzibar: Maswali yajitokeza


Makaburi yaliyochimbwa kuzika waliofariki katika ajali ya meli Zanzibar.
Makaburi yaliyochimbwa kuzika waliofariki katika ajali ya meli Zanzibar.

Uzito uliosababishwa na watu na mizigo yakiwemo magari na vifaa vya ujenzi huenda ulisababisha meli hiyo kuzama

Juhudi za uokozi au upatikanaji wa maiti zaidi ziliendelea Jumapili kufuatia ajali ya MV Spice Islander Ijumaa usiku, huku maswali yakiwa yameanza kujitokeza kwa nini ajali hiyo ilitokea.

Mpaka Jumapili hakukuwa na idadi ya uhakika wa watu waliokufa katika ajali hiyo ingawa matamshi mengi rasmi yalitaja idadi ya zaidi ya watu 200. Lakini maafisa wa serikali na maswala ya usafiri mpaka sasa hawajaweza kutoa hakika hasa meli ile ilikuwa imebeba watu wangapi. Kwa hiyo hata kuwa na uhakika wa waliofariki inakuwa vigumu.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema kupitia Waziri katika Ofisi ya Makamu wa pili wa Rais, Mohammed Aboud Mohamed kuwa hatua zitachukuliwa kwa wote itakaobainika walifanya uzembe uliosababisha kuzama kwa meli ya MV Spice.

Akizungumza na waandishi wa habari Waziri Mohammed alisema juhudi za serikali bado ziko katika kazi za uokoaji na kubainisha waliofariki.

Tanzania iko katika siku tatu za maombolezo, hali iliyosababisha Rais Jakaya Kikwete kufuta ziara yake ya kwenda nchini Canada mapema wiki hii.

Ripoti za awali zinasema meli hiyo ilikuwa imebeba watu 200 zaidi ya kiwango chake cha kawaida, pamoja na mizigo yakiwemo magari na vifaa vya ujenzi.

XS
SM
MD
LG