Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 12:39

Ali Bongo ateuwa serikali mpya


Rais mpya wa Gabon Ali Ben Bongo ameteuwa maafisa wa kwanza wa serikali yake. Bwana Bongo anaahidi mabadiliko baada ya uongozi wa zaidi ya miaka 40 wa marehemu babake, Omar Bongo.

Paul Mba ataendelea kufanya kazi kama kaimu waziri mkuu huku Paul Tongui akishikilia wadhifa wake kama waziri wa mambo ya nje. Jean Francois Ndoungou pia ataendelea na wadhifa wake kama waziri wa maswala ya ndani.

Naye Bi Angelique Ngoma amehamishwa kutoka wizara ya maswala ya kijamii na kupewa wadhifa wa waziri wa ulinzi. Hii ni mara ya kwanza kwa mwanamke kupewa wadhifa kama huo nchini Gabon. Rais Bongo alikuwa waziri wa ulinzi wakati wa utawala wa babake Omar Bongo aliyeaga dunia mwezi Juni.

Mawaziri wote 12 katika serikali hii mpya ni wakongwe wa kisiasa waliokuwa katika utawala wa zamani lakini rais Bongo amepunguza idadi ya wizara. Serikali yake mpya ina maafisa 30 akiwemo yeye na waziri mkuu. Utawala wa babake ulikuwa na maafisa 44.

Francois Engongah Owono ni Katibu mkuu katika ofisi ya rais Francosis Engongah owono anasema serikali mpya ni ndogo na inajumwisha watu wenye dhamira kuona kwamba raia wote wa Gabon wanashirikiana kwa manufaa ya taifa lao.

Bwana Bongo aliapishwa jumamosi baada ya kipindi kirefu cha ukaguzi wa kura ya mwezi Agosti ilomleta mamlakani. Anaahidi kuimarisha mfumo wa afya, elimu na makazi nchini Gabon na kujaribu kugawa sawa raslimali za mafuta. Chini ya utawala wa babake Gabon ilikuwa ya sita katika orodha ya nchi zinazouza mafuta kwa wingi lakini asili mia 70 ya raia wake wanaishi maisha ya ufukara.

XS
SM
MD
LG