Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 03:25

Clinton atoa wito  kwa jumuia ya kimatiafa kuisaidia Somalia


Akimaliza ziara yake ya siku mbili nchini Kenya, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Hillary Clinton, alikutana kwa mara ya kwanza na Rais wa serikali ya mpito ya Somalia, Sheikh Sharif Sheikh Ahmed katika ubalozi wa Marekani mjini Nairobi.

Baada ya mazungumzo yao ya faragha ya saa mbili mwanadiplomasia wa juu wa Marekani aliwaambia waandishi wa habari kwamba Marekani inaamini serikali ya mpito inayoongozwa na Rais Sharif, TGF inatoa nafasi na matumaini mazuri kupambana na siasa kali na kurudisha utulivu katika taifa hilo la pembe ya Afrika, ambalo halijawa na serikali kuu inayofanya kazi tangu 1991.

Bi Clinton amesema kiongozi huyo wa Somalia anahamu sana kupata msaada wa dharura na wa usalama kutoka jumuia ya kimataifa ili maisha ya kawaida yaweze kurudi Somalia. "niliridhika sana kutokana na kwamba Sheikh Sharif aliomba msaada ili kuwarudisha watoto shule na vifaa vya afya ili kufungua tena hospitali na kuwapatia wasomali waliokua wanataabika sana huduma wanazo stahili kupata."

Waziri huyo wa Marekani alisifu pia kazi za jeshi la kulinda amani la Umoja wa Afrika AMISOM, akisema marekani imetoa dola milioni 150 mnamo miaka miwili iliyopita kusaidia kazi za kulinda amani na kuahidi msaada zaidi kupanua kazi zao.

Wakati huo huo Bi Clinton aliituhumu jirani wa Somalia upande wa kaskazini, Eritrea kwa kuwasaidia fedha na silaha wapiganaji wa Al-Shabab. Alisema Marekani itachukua hatua dhidi ya serikali ya Asmara ikiwa ni pamoja na kuiwekea vikwazo ikiwa vitendo hivyo vitaendelea .

XS
SM
MD
LG