Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini amekosolewa vikali na chama cha upinzani nchini humo, Democratic Alliance (DA) pamoja na makundi mengine, baada ya serikali yake kukataa kutoa ripoti ambayo inadhaniwa kuwa inalihusisha jeshi la Zimbabwe na ghasia zilizofuatia uchaguzi mkuu wa nchi hiyo.
Wakati Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Thabo Mbeki alipokua mpatanishi wa mzozo wa Zimbabwe, aliteua tume ya majenerali 6 wastaafu kuchunguza tuhuma za mateso na ukandamizaji wa jeshi la Zimbabwe wakati wa ghasia zilizofuatia uchaguzi wa nchi hiyo.
Baada ya uchunguzi huo tume ilimkabidhi Mbeki ripoti hiyo, lakini ofisi ya Rais Zuma imekataa kutoa ripoti ikidai kwamba hakuna ripoti kwa vile majenerali hawajamkabidhi ripoti iliyoandikwa.
Lakini chama kikuu cha upinzani cha Afrika Kusini, Democratic Alliance (DA), vyama vya siasa nchini Zimbabwe na mashirika yasiyo ya kiserekali Afrika Kusini, wanadai kuwa Rais Zuma anaficha ukweli wa mambo.