Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 02:14

Bush Apokea Tuzo ya Bishop T Walker


Rais George Bush ameungana na viongozi wengine waliopokea tuzo ya Bishop John T. Walker, ambayo hutolewa kila mwaka kwa viongozi au watu ambao wametoa mchango mkubwa kulisaidia bara la Afrika.

Rais Bush alitunukiwa tuzo hiyo kwa juhudi alizozifanya wakati wa utawala wake kwa kupambana na magonjwa katika bara la Afrika, na kupanua msaada wa maendeleo wa Marekani kupitia mradi wa Millennium Challenge, ambao unaambatana na msaada wa mageuzi ya kisiasa na kiuchumi.

Akipokea tuzo hiyo Jumatano alisema Marekani inawajibu wa kusaidia watu wa bara la Afrika.

Bwana Bush amesema, "Ni kwa maslahi ya usalama wetu wa kitaifa kupambana na ukosefu wa matumaini. Ni kwa maslahi yetu ya kiuchumi tusaidie ukuaji wa uchumi. Na ni kwa masiliahi yetu ya kinidhamu kwamba tunapogundua njaa na ufukara , Marekani ijibu kwa nguvu na kwa haraka."

Tuzo hiyo ilitolewa na taasisi ya Africare, ambayo inashughulikia matatizo yanayoikabili Afrika, na kuratibu miradi katika maeneo tofauti kuanzia maji safi, hadi huduma za wakimbizi.

Dhifa rasmi ya Africare hapa Washington, ni miongoni mwa matukio makubwa yanayofanyika kila mwaka hapa Marekani kwa ajili ya bara la Afrika, ambapo inawakutanisha pamoja zaidi ya maafisa elfu moja wa serikali za kimataifa na wafanyabiashara.

Rais pia alielezea juu ya watu waliopokea siku za nyuma tuzo ya Africare ya Walker na kusema yeye sasa ni miongoni mwa watu wazuri, ambao ni pamoja na rais wa zamani wa Afrika ya Kusini Nelsoin Mandela, rais wazamani wa Marekani Jimmy Carter na Bill Clinton na rais wa Liberia Ellen Johnson Sirleaf.
XS
SM
MD
LG