Mshauri mkuu wa Umoja Mataifa anasema serikali ya mpito ya Somalia haipendelei kuwa na mahakama maalum katika nchi nyingine za kuwafanyia mashtaka maharamia wa Somalia. Patricia O’Brien aliliambia baraza la usalama la Umoja Mataifa kwamba Somalia imesema inapendelea mahakama kama hiyo kuanzishwa huko Somalia na kwamba wako tayari kufanya kazi kwa pamoja na Umoja Mataifa katika kukubaliana juu ya wapi pa kufungua mahakama hiyo.
Kwa muda sasa,Umoja Mataifa umekuwa ukitafakari wazo la kuwa na mahakama maalum kushughulikia watuhumiwa wa uharamia. Wamekuwa na mapendekezo kadhaa ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa mahakama hiyo huko Somalia.
Kulingana na ripoti ya umoja wa mataifa, kuna watuhumiwa wa uharamia zaidi ya elfu moja ambao wameshikiliwa katika nchi 20. Wengi wao wamehukumiwa katika mahakama za nchi hizo ikiwa ni pamoja na Kenya, Uholanzi, Marekani, Tanzania, Yemen na Oman.
Lakini Somalia ina idadi kubwa zaidi ya washukiwa wa uharamia walioko kizuizini na inasikiliza kesi nyingi za uharamia.